Wednesday, August 10, 2011

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 9/08/2011 BUNGE KUCHUNGUZA UFISADI UDA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
9/08/2011
BUNGE KUCHUNGUZA UFISADI UDA

Ndugu Wanahabari, Suala la Ubinafsishaji wa Shirika la UDA limeibua hisia kali miongoni mwa
Wabunge, vyombo vya habari na wananchi kwa ujumla. Suala hili limekuwa tata na kuzusha kila
aina ya maneno. Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma imeona ipo haja ya msingi
ya suala hili kuchunguzwa kwa kina na mhimili wa Bunge.
Kwa hiyo, imemuandikia barua Spika wa Bunge, ikimuomba aridhie mapendekezo ya wabunge
watakaoundakamati ndogo ya Bunge chini ya Kamati hii ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za
Mashirika ya Umma, ili ichunguze sakata zima la uuzwaji wa Shirika la UDA.
Uchunguzi huu umependekezwa kufuatia hisia kwamba taratibu za kuuza Shirika hili pamoja na
mali zake hazikuzingatia Sheria za nchi na hivyo kupelekea Taifa kuwa katika hatari ya kupoteza
mali.
Kwa mujibu wa Kanuni za Bunge Toleo la mwaka 2007, nyongeza ya sita kifungu cha 13(e),
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ina jukumu la kufuatilia ‘Utekelezaji wa Sera
ya Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma’ na kanuni ya 13(d) ‘kufanya tathmini ya ufanisi wa
Mashirika ya Umma’. Ili kutekeleza majukumu haya, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma
imemuomba Mhe. Spika aridhie kuundwa kwa kamati ndogo ili kufanya uchunguzi wa suala la
Shirika la UDA.
Hadidu Rejea
Hadidu rejea za Kamati ndogo ya uchunguzi inayopendekezwa ni kama ifuatavyo:
i. Kuchunguza kama katika zoezi la kubinafsisha Shirika la UDA taratibu zote za Sheria
zilifuatwa.
ii. Kuchunguza kama Ofisi ya Msajili wa Hazina na Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma
(CHC) walitimiza wajibu wao ipasavyo katika zoezi zima la ubinafsishaji wa Shirika la
UDA.
iii. Kuchunguza kama Bodi ya Shirika la UDA ilifuata sheria na kanuni katika kuuza hisa
zilizouzwa za Shirika la UDA na kama walikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo bila
kuhusisha wana hisa. Pia kuchunguza nafasi ya Bodi kwa umoja wake na mjumbe mmoja
mmoja wa Bodi katika zoezi zima husika.
iv. Kuchunguza nafasi (role) ya wana hisa (Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na Serikali)
katika zoezi zima la kuuzwa kwa hisa (unalloted shares) za UDA kwa Kampuni ya Simon
Group.
v. Kuwaita mbele ya Kamati wadau wote wa suala la UDA hususani Bodi ya UDA
iliyokuwepo, Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam,
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la UDA, Mmiliki wa Kampuni ya Simon Group ltd,
Msajili wa Hazina, Mkurugenzi Mkuu wa CHC, Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi na mtu
mwingine yeyote yule itakavyoonekana inafaa.
vi. Kufanya tathmini ya Shirika la UDA katika mazingira ya sasa ya biashara ya usafirishaji
Jijini Dar es Salaam.
vii. Kutoa Mapendekezo ya hatua za kuchukua dhidi ya watakaobainika kuwa na makosa
katika zoezi zima la Ubinafsishaji wa Shirika la UDA.
viii. Kupendekeza namna bora ya kuendesha Shirika la UDA.
Ukomo
Kwa kuwa mamlaka nyingine za Uchunguzi zinaendelea na uchunguzi wake, Kamati hiyo ya
Bunge itajikita katika maeneo yaliyoainishwa hapo juu tu na haitahusika na suala kama la
rushwa au Mahesabu ambayo yanashughulikiwa na TAKUKURU na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu
wa Hesabu za Serikali.
Isipokuwa Kamati inaweza kuhitaji msaada wa Taasisi hizi katika kutimiza wajibu wake wa
uchunguzi wa kibunge. Bunge, kwa namna yoyote ile, halitazuiwa kuendelea na uchunguzi wake
wakati Serikali (Executive) ikitimiza wajibu wake. Izingatiwe kuwa uchunguzi huu pia unahusisha
Taasisi za Serikali zenye mamlaka ya masuala ya Ubinafsishaji na utunzaji wa Mali ya Umma
(hivyo Serikali pia inachunguzwa).
Muda wa Uchunguzi
Nimependekeza kuwa uchunguzi huu uchukue jumla ya Siku 14 (kumi na nne tu) na kuwasilisha
taarifa yake kwa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma na kisha kwa Spika ambaye
ataelekeza hatua zitakazofuatia.
Wajumbe wa Kamati Ndogo ya Uchunguzi.
Kwa kuwa Uchunguzi huu unahusisha mambo mengi, nimependekeza kamati hiyo ndogo
ihusishe Wabunge wengine katika uchunguzi huu badala ya wajumbe wa Kamati ya Mashirika
ya Umma peke yake.
Wajumbe wafuatao wanapendekezwa kuunda Kamati ndogo.
1. Mhe. Murtaza Mangungu, Kilwa Kaskazini (Kamati ya POAC) – Mwenyekiti
2. Mhe. Esther Bulaya, Viti Maalum (Kamati ya POAC)
3. Mhe. Amina Mwidau, Viti Maalumu (Kamati ya POAC)
4. Mhe. David Kafulila, Kigoma Kusini (Kamati ya LAAC)
5. Mhe. Angellah Kairuki, Viti Maalumu (Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala)
6. Mhe. Herbert Mtangi, Muheza (Kamati ya Miundombinu)
7. Mhe. John Mnyika, Ubungo (Mwakilishi Wabunge wa Dar es Salaam)
Katibu wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma na Katibu wa Kamati ya Sheria ndogo
wanapendekezwa kuwa Makatibu wa Kamati ndogo ya Uchunguzi wa Ubinafsishaji wa
Shirika la UDA.
Ni matarajio yangu na ya wenzangu kuwa Spika wa Bunge, Mhe.Anne Makinda ataridhia
kuundwa kwa Kamati hiyo, ili Bunge liweze kuchukua wajibu wake wa kiuchunguzi na wa
kuisimamia Serikali. Ninaamini, uchunguzi huo ndio utakaokata mzizi wa fitina kuhusu nani
amehusika na achukuliwe hatua gani zichukuliwe kwa maslahi ya Wakazi wa Jiji la Dar es
Salaam na Taifa zima kwa ujumla.
Nashukuru kwa kunisikiliza.
Kabwe Zuberi Zitto (Mbunge)
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma

No comments: